Monday 4 May 2015

maambukizi ya ukimwi yatishia uhai kwa watoto

Bagamoyo.
 Maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto yameelezwa kuwa tishio na asilimia 50 ya watoto wanaozaliwa na virusi vya ugonjwa huo hupoteza maisha ndani ya miaka miwili tangu kuzaliwa wasipopatiwa dawa za kupunguza makali ya virusi (ARV).
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi wa Shirika lisilo la kiserikali la EGPAF linalojishughulisha na harakati za kutokomeza maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, Dk Jeroen Van’t Pad Bosch, wakati akitoa mafunzo kwa waandishi wa habari yaliyolenga kuwajengea uwezo wa kuandika habari zihusuzo maambukizi ya Ukimwi toka kwa mama kwenda kwa mtoto.
Mkurugenzi huyo alisema miongoni mwa wanawake wajawazito 100 wenye virusi vya Ukimwi wasipopatiwa dawa, watoto wanaozaliwa asilimia 80 hupoteza maisha ndani ya miaka mitano na vifo vingi vinatokana na kinamama hao kutotii masharti wanayopewa wakati wa kliniki na baada ya kujifungua.
Alisema waandishi wa habari wana kila sababu ya kujikita katika kuandika habari za Ukimwi ili wananchi waone umuhimu wa kupima na kutumia dawa mapema.
Alisema licha ya elimu hiyo kutolewa kila mara, bado kuna watu hawaoni umuhimu wa kupima mapema.
Naye mtaalamu kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Grace Dennis alisema kiwango cha maambukizi kwa watoto nchini kimefikia asilimia 15.7 kwa takwimu za mwaka 2013, na kwa sasa Serikali imedhamiria kupunguza maambukizi hayo hadi kufikia asilimia nne ifikapo mwaka kesho.
Alisema changamoto iliyopo ni kwa wajawazito wanaojifungulia nyumbani kukosa nafasi ya kupima ili wapatiwe huduma zinazostahili mapema, ikiwamo ya dawa za ARV na huduma za uzazi salama ambazo wengi wao huzikosa.

No comments:

Post a Comment